GEITA YAKUSANYA MAPATO KWA ASILIMIA 125

 Halmashauri ya Wilaya ya Geita imefanikiwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato kwa mwaka wa fedha 2024/25 kwa asilimia 125.19 baada ya kukusanya jumla ya Shilingi bilioni 10.4 dhidi ya bajeti ya awali ya Shilingi bilioni 8.3. Hii ni zaidi ya Shilingi bilioni 2.1 kutoka makadirio ya awali.

 Hatua hiyo imechangiwa na usimamizi madhubuti wa mapato ya ndani pamoja na udhibiti wa mianya ya upotevu, ambapo watendaji wa halmashauri waliweka msukumo mkubwa katika uadilifu na ubunifu wa vyanzo vya mapato.

‎Kupitia mafanikio ya ukusanyaji wa mapato, Halmashauri iliweza kutenga Shilingi bilioni 3.1 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta za elimu, afya, miundombinu na utawala.

‎Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa shule mpya, zahanati, vituo vya afya, nyumba za watumishi pamoja na ofisi za kata.

‎Aidha, kwa kutekeleza agizo la Serikali la kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo, Halmashauri ilitoa mikopo yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.8 kwa makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu waliokidhi vigezo, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha kiuchumi.

‎Katika kuimarisha mapato ya siku zijazo, Halmashauri imeendelea kutwaa maeneo ya kimkakati kwa ajili ya uwekezaji.

‎Mnamo Julai 24, 2025, Timu ya Menejimenti ya Halmashauri ilifanya ziara katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro kukagua maeneo yanayotarajiwa kutwaliwa kwa uwekezaji.

‎Miongoni mwa maeneo hayo ni eneo lenye ukubwa wa hekari 14 litakalotumika kwa ujenzi wa kituo cha mabasi (Katoro Bus Stand) pamoja na soko la Kariakoo Katoro, hatua ambayo inalenga kuboresha mazingira ya biashara na kuongeza mapato.

‎Halmashauri ya Wilaya ya Geita inaendelea kutekeleza mikakati ya kuongeza mapato ya ndani ili kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi, huku ikiishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuipatia rasilimali na fedha kwa ajili ya shughuli za maendeleo.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form