KONGAMANO LA KISAYANSI LAFANYIKA KUBORESHA HUDUMA

 Hospitali ya Rufaa Mtakatifu Joseph Peramiho Yaendesha Kongamano la Kisayansi Kuboresha Huduma za Afya Ruvuma.

 Katika jitihada za kushirikiana na serikali katika kuboresha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi, Hospitali ya Rufaa Mtakatifu Joseph Peramiho iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma, imeandaa na kuendesha kongamano la kisayansi lililolenga kubadilishana uzoefu wa kitaaluma katika sekta ya afya.


Kongamano hilo limewakutanisha waganga wafawidhi kutoka vituo mbalimbali vya afya, hospitali za serikali pamoja na hospitali binafsi mkoani Ruvuma. Washiriki wameongozwa na madaktari bingwa kutoka hospitali hiyo, wakiwemo wataalamu wa magonjwa ya ndani na upasuaji, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi, hususan huduma za rufaa.

Akizungumza katika kongamano hilo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Dkt. Godfrey Kihaule, pamoja na Mkurugenzi wa Hospitali ya Peramiho, Dkt. Ansgar Tuffe, walisema kuwa kongamano hilo limekuwa jukwaa muhimu kwa watoa huduma za afya kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu mpya na za kisasa, ili kuboresha huduma za kinga na tiba kwa wananchi wa mkoa wa Ruvuma.

Kwa upande wao, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mtakatifu Joseph Peramiho, Dkt. Deodatus Haule, na Daktari Bingwa wa Upasuaji, Dkt. Jafeth Mfinanga, walieleza kuwa kupitia kongamano hilo, washiriki wamepata uelewa mpana kuhusu huduma za kibingwa zinazotolewa hospitalini hapo. Walisema hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza idadi ya wananchi wanaolazimika kusafiri kwenda mikoa mingine kufuata huduma hizo.

Kongamano hili ni sehemu ya juhudi za pamoja kati ya sekta binafsi na ya umma katika kuimarisha mifumo ya afya na kuhakikisha huduma zinapatikana kwa wakati na kwa ubora unaohitajika.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form