MKUU WA MKOA MOROGORO AKAGUA UCHIMBAJI WA VISIMA

 MKUU wa mkoa wa Morogoro,Adam Malima amefanya ukaguzi wa zoezi la uchimbaji visima vya maji safi na salama ndani ya manispaa ya Morogoro eneo la kata ya Mafisa ikiwa ni sehemu ya maendeleo na kuhakikisha wananchi wa manispaa hii wanapatiwa mahitaji muhimu.

Serikali kwa kushirikiana na Bodi ya Maji Bonde la Wami/Ruvu, Mamlaka ya Maji safi na usafi wa Mazingira Morogoro(MORUWASA) na Wakala wa Maji na usafi wa Mazingira vijijini (RUWASA) imeendelea kutatua changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa kuchimba visima kwenye maeneo mbalimbali ya Manispaa ya Morogoro.

Juhudi hizo zimeelezwa kuwa ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya Maji safi na salama kwa urahisi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa uchimbaji wa mojawapo ya kisima kilichopo Kayenzi, Kata ya Mafisa, chenye urefu wa mita 120, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima amesema kisima hicho kitapunguza kwa kiwango kikubwa tatizo la maji kwani kitawanufaisha wakazi zaidi ya Laki moja.

Malima ameendelea kusisitiza umuhimu wa kulinda maeneo ya visima kwa kuyatambua kama hifadhi za maji ambapo ameelekeza mamlaka husika kuhakikisha wananchi wanaoishi karibu na maeneo ya miradi hiyo wanalipwa fidia stahiki na kuhamishiwa maeneo mengine ili kuruhusu utekelezaji wa miradi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Wami/Ruvu, Elibariki Mmasy, ameeleza tayari wamebaini jumla ya maeneo 17 yenye vyanzo vya kuchimbwa visima ambapo 7 tayari vimechimbwa na vimeonyesha matokeo chanya.

Naye, Meneja (RUWASA) Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Sospeter Lutonja, amesema kuwa hadi sasa jumla ya visima 66 vimechimbwa katika mkoa huo.







 

 

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form