KANISA LA GWAJIMA LAOMBA MSAADA WA SULUHU THRDC

 KANISA la Ufufuo na Uzima, linaloongozwa na Askofu Josephat Gwajima, limeuomba Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) kushiriki katika jitihada za kutafuta suluhu ya mvutano unaoendelea kati ya kanisa hilo na mamlaka, ili liweze kurejea katika shughuli zake za kiibada kama kawaida.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasili katika ofisi za THRDC jijini Dar es Salaam, Askofu Amos Paul, kwa niaba ya uongozi wa kanisa hilo, alisema kuwa sintofahamu iliyopo kwa sasa imewalazimu kutafuta msaada wa mtandao huo wa Watetezi wa Haki ili kuhakikisha Haki yao ya kuabudu inalindwa.

Amesema kuwa hali hiyo imezua wasiwasi mkubwa miongoni mwa waumini, hasa kutokana na hatua zilizochukuliwa na askari polisi kuondoa waumini kwa nguvu na kuzuia kuendelea kwa ibada katika baadhi ya matawi ya kanisa hilo.

Kwa upande wake, Wakili Onesmo Olengurumwa, Mratibu Kitaifa wa THRDC, ametoa wito kwa Waziri wa Mambo ya Ndani pamoja na Jeshi la Polisi kukaa meza moja na uongozi wa kanisa hilo kwa lengo la kuhitimisha mvutano huo kwa njia ya mazungumzo ya amani.

Mgogoro kati ya Kanisa la Ufufuo na Uzima na mamlaka umeibuka kufuatia kile kinachodaiwa kuwa ni ukiukwaji wa taratibu za usajili na uendeshaji wa taasisi za kidini, madai ambayo kanisa hilo limekana na kudai kuwa yanatumika kama kisingizio cha kulizuia kuendesha ibada.

Katika siku za hivi karibuni, askari polisi walivamia baadhi ya matawi ya kanisa hilo na kuzuia ibada kuendelea, huku wakiondoa waumini kwa nguvu, hatua iliyozua taharuki na malalamiko kutoka kwa viongozi wa dini na wanaharakati wa haki za binadamu.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form