MGOMBEA UBUNGE UKONGA AAHAIDI EXCAVATOR TATU

Mgombea Ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Jimbo la Ukonga, Ndugu Alawi Abdallah Rwegoshora, ameibuka kuwa mmoja wa wagombea wenye ushawishi mkubwa zaidi katika kinyang’anyiro cha kura za maoni, kufuatia ahadi zake zenye mwelekeo wa maendeleo makubwa kwa wakazi wa jimbo hilo.
 
Ndugu Alawi, ambaye pia ni Katibu wa Jumuiya ya Watanzania waishio China, ameweka bayana dhamira yake ya kuliletea Ukonga mabadiliko kupitia miradi yenye tija.

Miongoni mwa ahadi kubwa alizotoa ni upatikanaji wa mashine tatu za kuchimba barabara (Excavator 3) - yatakayotumika kuboresha miundombinu ya barabara ndani ya jimbo hilo, hatua itakayopunguza changamoto za usafiri na kuimarisha huduma za kijamii na kiuchumi.

Aidha, ameahidi kutoa fursa za elimu kwa vijana watatu kila mwaka kwa kuwapeleka kusoma shahada nje ya nchi kupitia ushirikiano wake na taasisi mbalimbali za kimataifa; hatua hiyo inalenga kuongeza idadi ya vijana waliobobea kitaaluma na kurudi kulijenga taifa.

Katika eneo la uchumi, Alawi ameweka mkazo kwenye ujenzi wa soko jipya la kisasa katika eneo la Gongolamboto ambapo mchakato wa awali wa utekelezaji umeshaanza kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo kutoka ndani na nje ya nchi.

Mradi huo unalenga kuinua wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wa eneo hilo.

Kwa mujibu wa Alawi, jitihada hizo ni za kibinafsina hazitegemei fedha za Serikali au bajeti ya jimbo, jambo ambalo limeongeza imani ya wananchi kwa mgombea huyo kutokana na moyo wake wa kizalendo na kujitolea.

Alawi ametoa ahadi hizo katika majukwaa mbalimbali ya kampeni ya kuelekea mchakato wa kura za maoni wa CCM unaotarajiwa kufanyika kesho, tarehe 04 Agosti 2025.

Sera zake zenye mvuto kwa jamii zimeibua ari mpya na hamasa kubwa miongoni mwa wajumbe wa chama na wananchi kwa ujumla.

Jimbo la Ukonga sasa limewaka moto huku jina la Alawi Abdallah likitajwa kama chaguo la wengi kuelekea Uchaguzi Mkuu ujao.



 

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form