TANAPA YAPOKEA TUZO KUSAIDIA WATU WENYE ULEMAVU

 Katika tukio la kihistoria lililojawa na hisia za shukrani na heshima, taasisi isiyo ya kiserikali ya Foundation for Disabilities Hope (FDH) imetunuku tuzo maalumu kwa Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), CPA (T) Musa Nassoro Kuji, kwa niaba ya shirika hilo, ikiwa ni kutambua mchango mkubwa wa TANAPA katika kuendeleza huduma jumuishi kwa watu wenye ulemavu nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika leo, Julai 18, 2025, katika ukumbi wa mikutano wa TANAPA jijini Arusha, Mkurugenzi Mtendaji wa FDH, Bw. Maiko Salali, alieleza kuwa TANAPA imekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha watu wenye ulemavu wananufaika ipasavyo na vivutio vya utalii pamoja na huduma jumuishi ndani ya Hifadhi za Taifa.

"Upendo wenu umeleta mabadiliko chanya na umechipua mizizi ya mafanikio yaliyojengwa sanjari na nia yenu njema kwa watu wenye ulemavu," alisema Bw. Salali.

Aidha, aliongeza kuwa mchango wa TANAPA umechangia si tu katika ustawi wa kijamii bali pia katika kuinua uchumi wa watu wenye ulemavu kupitia fursa mbalimbali zinazotolewa na shirika hilo.

 "Tunatambua na kuthamini sana juhudi zenu. TANAPA ni mfano wa kuigwa kwa kufanya huduma zake kuwa jumuishi. Tunapokuja TANAPA, tunajisikia tuko nyumbani. Maono ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kusaidia watu wenye ulemavu mnayaendeleza kwa vitendo," alisisitiza Bw. Salali.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, CPA (T) Musa Nassoro Kuji, alieleza kuwa dhamira ya shirika ni kuhakikisha mazingira ya hifadhi yanakuwa rafiki kwa watu wote bila ubaguzi.

"Kuweka mazingira rafiki na jumuishi kwa watu wote ndiyo dhamira kuu ya TANAPA, na tutaendelea kufanya hivyo kwa mustakabali wa Taifa letu," alisema Kamishna Kuji.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Massana Mwishawa, maafisa waandamizi wa TANAPA, askari wa uhifadhi pamoja na wawakilishi waandamizi kutoka FDH.






 

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form