MAAFISA MAENDELEO WAPIGWA MSASA ASILIMIA 30 ZABUNI ZA UMMA

 Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), imeandaa mafunzo kwa ajili ya kuwajengea uwezo Maafisa Maendeleo ya jamii kutoka ngazi ya kata hadi mkoa, mkoani Iringa kwa lengo la kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kunufaika na fursa ya asilimia 30 ya zabuni za umma. 

 
Akifungua mafunzo hayo Julai 11, 2025 katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa M, Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Felista Mdemu, amesema serikali imedhamiria kuhakikisha makundi maalum yanashiriki kikamilifu katika mifumo rasmi ya uchumi kwa kutumia fursa ya asilimia 30 ya zabuni zilizotengwa kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya Umma, Sura 410.


"Serikali imefungua milango, na sasa tunahitaji kuona maafisa maendeleo ya jamii wakichukua nafasi ya kuwa walimu na washauri wa vikundi ili viweze kujisajili, kujiandaa na kushiriki katika zabuni hizo," amesema Mdemu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Jamii, Patrick Golwike, amefafanua kuwa changamoto kuu kwa makundi maalum si ukosefu wa fursa, bali ni maandalizi duni, ukosefu wa nidhamu ya kibiashara na kutokuelewa taratibu za kushiriki zabuni.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Jamii, Juliana Kibonde, alisema kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuwajengea uwezo maafisa maendeleo ya jamii ili waweze kuhamasisha uundwaji wa vikundi vipya na kuviunganisha na mifumo rasmi ya manunuzi na uchumi.'

Katibu Tawala Msaidizi wa Mkoa wa Iringa, Venance Ntyarundula, amesema kuwa mkoa umejipanga kuandaa kongamano la kila mwaka la maafisa maendeleo ya jamii, ili kutathmini utekelezaji wa sera na programu zinazolenga kuboresha maisha ya makundi maalum.

"Tunaanza mwaka huu wa fedha kwa mtazamo mpya. Tunataka kuona vikundi vikipewa zabuni, wakipata mapato, na hatimaye kubadilisha maisha yao. Hii ni njia ya kuhakikisha hakuna mwananchi anayebaki nyuma katika maendeleo ya taifa," amesema Ntyarundula.





 

Post a Comment

Previous Post Next Post

Contact Form