KILIO CHA MAMA CHAMSUKUMA MHE.MAVUNDE KUCHUKUA HATUA,MTANZANIA AACHIWA SUDAN KUSINI

 Na Ally Mandai

 Anaandika Mbunge wa Jimbo la Mtumba na Waziri wa Madini Mhe.Anthony Mavunde.

Mwezi September 2025 nikiwa katika Mtaa wa Sogeambele,Kata ya Chihanga-Dodoma kwenye Kampeni ya Mtaa kwa Mtaa nikakutana na Mama mmoja ambaye aliomba kuniuliza swali lakini baada ya kupewa 𝙈𝙖𝙞𝙠𝙞 hakuuliza swali na badala yake aliangua kilio kikali akiniomba nimsaidie mwanaye Juma Maganga aliye gerezani Juba,Sudan Kusini arejee uraiani na kuja kuungana na familia yake.

Juma ni dereva wa magari makubwa ambaye akiwa Sudan Kusini Tarehe 14.02.2025 alipata ajali ya kumgonga Mwanajeshi mmoja ambaye alipoteza maisha yake na hivyo kupelekewa Juma kushikiliwa na vyombo vya sheria Sudan na kuhitajika kulipa faini ya ng’ombe 51 sawa na Tsh 36,000,000 kwa mila na desturi ya Sudan inapotokea ajali inayosababisha kifo kwa kuwa marehemu alikuwa ameacha wake watatu na hivyo lazima wote wafikiwe na mgao pamoja na wazazi wake.
Taratibu za kuchangishana ziliendelea na kupitia watanzania waliopo Juba na hapa nchini tulijitahidi kumchangia kumaliza changamoto hiyo lakini fedha hiyo haikufika lengo na kumfanya Juma aendelee kusota gerezani kwa miezi 10 huku akiwa amefungwa minyororo muda wote.

Sikujua kama yule ni mama mzazi wa Juma lakini nikamjulisha Mama kwamba nalifahamu tatizo la mwanaye na tunaendelea kumsaidia,nikampa taarifa tu kwamba kwa muda wote akiwa gerezani;

-Namsaidia Chakula chake kule Sudan

-Naisaidia Familia yake iliyopo hapa Dodoma kupata mahitaji muhimu.

Nikamtia moyo Mama kwamba Juma atatoka tumepata ushirikiano mkubwa wa serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na wakati Juma aliniambia inahitajika Dola 2000 ili aachiwe huru fedha ambayo niliituma Mahakamani Sudan kumsaidia kutoka lakini kwa bahati mbaya fedha ile haikusaidia kumtoa Juma na aliendelea kushikiliwa.

Wiki iliyopita Mtanzania mmoja aitwaye Nickson alinipigia simu na kunijulisha kwamba wamejiridhisha kwamba ikipatikana Dola 1500 ziada ya ile ya awali Juma ataachiliwa.

Tulifanya malipo ya Dola 1500 kule Mahakama ya Juba,Sudan tarehe 29.12.2025.

Jana Tarehe 31.12.2025 Juma ameachiliwa na sasa yupo njiani kurejea Nyumbani Dodoma,Tanzania.

Natumai Mama na Mke wa Juma siku ya leo itakuwa siku kubwa ya kumshukuru Mungu kwa matendo makuu aliyowatendea.


 

Post a Comment

0 Comments