WATU 29 MBARONI KWA MAUAJI KISA KUIBIWA NYETI-RUKWA

Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa linawashikilia watu 29 kwa tuhuma za kuhusika na tukio la Mauaji lililotokea katika Kijiji cha Madibila, Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa, baada ya kuzuka kwa vurugu zilizodaiwa kuchochewa na taarifa za uongo kuhusu kuibiwa kwa Nyeti.
 

Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi, tukio hilo lilitokea Agosti 20, 2026, majira ya saa 12:45 jioni, baada ya Vijana saba kufika kijijini hapo kwa ajili ya kutoa huduma za usajili wa laini za simu.

Wakati wakiendelea na shughuli hiyo, kulitokea taharuki baada ya Mwananchi mmoja aitwaye Mpaji Simkanji kudai kuwa alikuwa ameibiwa Nyeti zake. Madai hayo yalisababisha baadhi ya Wananchi kuanza kuwashambulia vijana hao kwa kutumia mawe, fimbo na silaha nyingine za jadi.

Katika vurugu hizo, kijana mmoja, Devid Amos Mwimanz, mwenye umri wa miaka 22, mkazi wa Kijiji cha Kasanga, aliuawa na wenzake wengine kujeruhiwa maeneo mbalimbali ya miili.

Polisi pia imesema wananchi hao walichoma moto gari aina ya Nissan lenye namba za usajili T.157 DQP, lililokuwa likitumiwa na vijana hao kwa usafiri.

Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi ili kubaini hatua zaidi za kisheria dhidi ya watuhumiwa hao.

Aidha, Jeshi hilo limetoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kuendekeza imani za kishirikina na kujichukulia sheria mkononi, likieleza kuwa vitendo hivyo vinaweza kusababisha madhara makubwa kwa jamii.

Post a Comment

0 Comments