Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewakosoa
wanaodai kuwa Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Bwawa la Mwalimu Julius
Nyerere (JNHPP) ni “white elephant” na kwamba hauna tija kwa Taifa,
akisisitiza kuwa ujenzi wa njia kuu za kusafirisha umeme unaendelea kwa
kasi kubwa ili kuhakikisha umeme unaozalishwa unafikishwa kwenye maeneo
mbalimbali nchini.
Akizungumza Jumamosi, Agosti 22, 2026, Mkoani
Pwani mara baada ya kuzindua mradi huo, Rais Samia alisema Tanzania
inaendelea kuvutia uwekezaji, jambo linaloongeza mahitaji ya umeme kwa
kasi. Alisema akiba ya umeme iliyopo sasa inaweza isiwe ya kutosha
katika miaka michache ijayo, hivyo Serikali inaendelea kuwekeza katika
vyanzo vingine vya nishati ikiwemo jua na upepo.
Rais Samia
alisema madai kwamba mradi huo ni “tembo mweupe” hayana msingi, akieleza
kuwa changamoto iliyokuwepo ya miundombinu ya kusafirisha umeme
inashughulikiwa kwa kasi. “Ujenzi wa njia za kusafirisha umeme
unaendelea kwa kasi kubwa na mradi huu ni mradi wa manufaa makubwa kwa
Taifa na si kama wanavyosema,” alisema.
Aidha, Rais Samia
alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha mradi huo unakuwa endelevu kwa
kutunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji vinavyoupa uhai, akiilekeza
Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu
kuratibu na kusimamia kwa karibu uhifadhi wa mazingira na vyanzo vyote
vya maji, hususan vile vinavyohusiana na mradi huo.
Alisema
jukumu la kulinda mazingira na vyanzo vya maji ni la kila mmoja,
akisisitiza kuwa hatua hizo ni muhimu ili kuhakikisha Bwawa la Mwalimu
Julius Nyerere linaendelea kutoa manufaa kwa Taifa kwa miaka mingi
ijayo.
0 Comments