Waziri, Dkt.
Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania kuendelea kuliombea Taifa na
kudumisha amani, akisema amani ni msingi unaowezesha wananchi, taasisi
za dini na Taifa kwa ujumla kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo.
Amesema
dunia inaendelea kushuhudia mabadiliko na mitikisiko katika maeneo
mbalimbali, hivyo kuna umuhimu wa kuendelea kumwomba Mungu ailinde
Tanzania na kuendeleza amani ambayo imeiwezesha nchi kutekeleza shughuli
zake kwa utulivu.
Waziri Mkuu amesema hayo leo (Jumapili, Agosti
23, 2026) aliposhiriki ibada katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri
Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mashariki na Pwani (DMP), Usharika wa
Kijitonyama, jijini Dar es Salaam.
“Tuendelee kuiombea nchi yetu.
Leo hii tunaweza kufanya ibada kwa sababu nchi yetu ipo na amani. Tuna
mipango mbalimbali kama nchi, katika ngazi ya familia, taasisi, Dayosisi
na Kanisa, lakini hayo yote tunaweza kuyafanya kama nchi yetu ipo na
amani,” amesema.
Dkt. Mwigulu amewafikishia waumini salamu za
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na
Serikali kwa ujumla, huku akitambua na kuenzi mchango mkubwa unaofanywa
na Kanisa katika maendeleo ya nchi.
Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za kidini katika kuhakikisha Tanzania inaendelea kusonga mbele.
“Hauwezi ukataja maendeleo ya nchi yetu bila kutaja mchango wa Kanisa,” amesema.
0 Comments