RAIS WA ZIMBABWE ASAINI SHERIA YA KUKAA MADARAKANI MIAKA 7

 Hatimaye Rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa amesaini kuwa sheria muswada unaoongeza muda wa urais kwa miaka miwili, hatua inayomruhusu kuendelea kuhudumu madarakani hadi mwaka 2030.

Msemaji wa Serikali ya Zimbabwe, Nick Mangwana, alithibitisha hatua hiyo, jana Jumanne Julai 7, 2026 kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa X, akisema: "Imesainiwa, imethibitishwa na sasa ni sheria," huku akiambatanisha nakala ya sheria hiyo.

Mwezi uliopita, mabunge yote mawili ya Zimbabwe yaliidhinisha muswada huo baada ya mjadala mkali ulioibua maoni yanayokinzana.

Wanaounga mkono hatua hiyo wanasema marekebisho hayo yatasaidia kupunguza gharama za kuandaa uchaguzi, huku wanaoupinga wakidai yanadhoofisha misingi ya demokrasia kwa kuwanyima wananchi haki ya kumchagua rais wao kupitia kura ya moja kwa moja.

Kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa na Idhaa ya Kiswahili BBC, sheria hiyo pia ina kipengele kinachoruhusu rais kuchaguliwa na Bunge badala ya wananchi kumpigia kura moja kwa moja.


 

Post a Comment

0 Comments