RAIS SAMIA ATEUA NA KUHAMISHA VIONGOZI HAWA

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi na uhamisho wa Viongozi mbalimbali. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka Jumatano Julai 22, 2026 kupitia Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, mabadiliko hayo yamehusisha uteuzi wa Naibu Makatibu Wakuu wapya ambapo Dkt. Latifa Mohammed Khamis kutoka TANTRADE ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia maswala ya Muungano.

Prisca Burton Lwangili kutoka TAMISEMI ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Aidha, mabadiliko hayo yamehusisha uhamisho wa Naibu Makatibu Wakuu kwenda katika sekta na wizara nyingine za kimkakati.

Katika hatua hiyo, Abdallah Hassan Mitawi amehamishwa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais kwenda Wizara ya Uchukuzi, huku Balozi Baraka Haran Luvanda akitolewa Ofisi ya Makamu wa Rais kwenda Wizara ya Katiba na Sheria.

Katika uteuzi huo Dkt. Franklin Jasson Rwezimula amehamishwa kutoka Wizara ya Katiba na Sheria kwenda Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, naye Dkt. Maduhu Isaac Kazi akihamishwa kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani kwenda Ofisi ya Makamu wa Rais kushughulikia masuala ya Mazingira.

Katika ngazi ya taasisi za serikali, Rais amemteua Ephraim Balozi Mafuru kuwa Mkurugenzi Mkuu mpya wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) akitokea Bodi ya Utalii Tanzania (TTB).


 

Post a Comment

0 Comments