MEYA JIJI LA DSM ASISITIZA USHIRIKIANO SEKTA YA ELIMU


Na Mwandishi wetu.

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam Mheshimiwa Nurdin Bilal amewataka wakuu wa shule katika Jiji hilo kushirikiana na Idara nyingine ili kurahisisha kazi za maendeleo katika sekta ya Elimu.

Ametoa wito huo wakati wa kikao kazi kilichowakutanisha wakuu wa shule za sekondari za Serikali na binafsi pamoja na maafisa elimu kata chenye lengo la kupanga mikakati ya kuanza muhula mpya wa masomo wa 2026.

Mhe.Nurdin amesema ili mipango ya Serikali iende kwa wakati, Idara ya Elimu haina budi kushirikiana na Idara nyingine huku akitolea mfano idara ya manunuzi na ujenzi.

"Nasisitiza ushirkishwaji katika utendaji wa kazi zenu na kwa nafasi yangu nitahakikisha nasimamia hili ili tuweze kusukuma mbele elimu yetu na kupata matokeo chanya". Alisema

Aidha amewasisitiza wakuu hao wa shule kutunza mali za Serikali zilizopo shuleni ili ziweze kuwahudumia wananchi wengi kwa muda mrefu.

Kikao kazi hicho kimefanyika siku moja baada ya muhula mpya wa masomo kwa mwaka 2026 kuanza rasmi Januari 13,2026 lengo likiwa ni  kumbushana kutimiza wajibu kwa kila mkuu wa shule na wadau wengine wa Elimu.


 

 

Post a Comment

0 Comments