Uwekezaji wa
shilingi bilioni 16 uliofanywa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa
Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) katika ununuzi wa pampu mpya nane
unatarajiwa kuongeza uwezo wa uzalishaji na usafirishaji wa maji, hatua
inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi wa Dar
es Salaam na Pwani.
Hayo yabainishwa, wakati wa ziara ya Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Mazingira na Maji, ikiongozwa na Mwenyekiti wake,
Mhe. Jackson Kiswaga, ilipotembelea na kukagua Mtambo wa Uzalishaji Maji
Ruvu Juu uliopo Mlandizi, Mkoa wa Pwani, kujionea hali ya uzalishaji,
uendeshaji pamoja na maendeleo ya ufungaji wa pampu hizo.
Kwa
mwananchi, uwekezaji huo unalenga kuongeza uwezo wa maji yanayochukuliwa
na kusafirishwa kutoka chanzo hadi mtamboni, hivyo kuwezesha DAWASA
kuzalisha na kusambaza maji kwa ufanisi zaidi.
Akizungumza baada
ya ziara hiyo, Mhe. Kiswaga amesema Kamati imeridhishwa na hatua
zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha miundombinu ya maji,
hususan uwekezaji katika pampu mpya unaolenga kuongeza ufanisi wa
huduma.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi
Mkama Bwire, amesema Mamlaka imenunua pampu mpya nane kwa gharama ya
shilingi bilioni 16. Kati ya hizo, pampu sita tayari zimewasili, huku
mbili zikiwa katika mchakato wa kuwasili.
Amesema pampu saba kati
ya hizo zimepangwa kufungwa katika Mtambo wa Ruvu Juu, ambapo nne
zitafungwa katika eneo la uchukuaji na usafirishaji wa maji ghafi, huku
tatu zikiwa zimepangwa kufungwa katika eneo la mtambo.
Kwa sasa,
pampu mbili tayari zimefungwa katika eneo la uchukuaji na usafirishaji
wa maji ghafi, huku nyingine mbili zikiwa zimefungwa katika eneo la
mtambo. Kazi ya kufunga pampu zilizosalia inaendelea.
0 Comments