JKCI YAFANYA UPASUAJI KWA MTOTO WA SIKU MBILI

 

Kwa mara ya kwanza, Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imefanikiwa kumfanyia upasuaji wa moyo bila kufungua kifua mtoto mwenye umri wa siku mbili tu aliyezaliwa akiwa na tatizo la kubana kwa mshipa unaopeleka damu kwenye mapafu. 

Upasuaji huo wa kihistoria kwa kutumia mtambo wa Cathlab umefanyika wakati wa kambi maalum ya siku sita iliyoendeshwa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na mradi wa Little Heart kutoka Shirika la Muntada Aid la nchini Uingereza.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa JKCI, Dkt. Angela Muhozya, ameeleza kuwa kambi hiyo imefanikisha upasuaji kwa jumla ya watoto 44, ambapo 28 walifanyiwa upasuaji kwa njia ya tundu dogo na 16 upasuaji mkubwa wa kufungua kifua, huku shirika hilo likichangia vifaa tiba vya thamani ya shilingi milioni 50.

Dkt. Angela ametoa rai kwa wajawazito na wazazi kufanya uchunguzi wa mapema wa magonjwa ya moyo kwa watoto ili kuokoa maisha yao na kuepuka kufika hospitalini wakati ugonjwa ukiwa umefikia hatua mbaya.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Muntada Aid, Nayaf Sheikh, amepongeza miundombinu bora na utaalamu wa JKCI akieleza kuwa ubora wa taasisi hiyo unaondoa ulazima kwa wananchi wa Tanzania na ukanda mzima wa Afrika Mashariki kusafiri nje ya nchi kufuata huduma za kibingwa za matibabu ya moyo.

Post a Comment

0 Comments