Mwanaume
mmoja katika mji wa Tamale, Mkoa wa Kaskazini nchini Ghana, amevutia
hisia baada ya kutumia mbinu ya kipekee ya kulinda nyumba yake dhidi ya
wezi kwa kuwapatia vijana wa eneo hilo huduma ya Wi-Fi bure.
Baada
ya kukamilisha ujenzi wa nyumba yake, mwanaume huyo alianza kutafuta
namna ya kupata mlinzi rasmi. Hata hivyo, kabla ya kuajiri mlinzi,
alibuni mkakati wa kuwavutia vijana wa eneo hilo kukusanyika karibu na
nyumba yake kila usiku.
Kwa kutumia router yake, aliweka huduma
ya intaneti inayopatikana kuanzia saa 11:00 jioni hadi saa 1:00 asubuhi
kila siku. Hatua hiyo iliwafanya vijana kutoka eneo hilo na maeneo ya
jirani kufika karibu na nyumba hiyo ili kutumia Wi-Fi hiyo bila malipo.
Vijana
hao waliamini kuwa mwenye nyumba alikuwa akiwapatia huduma hiyo kwa
ukarimu, bila kufahamu kuwa uwepo wao wa mara kwa mara ulikuwa ukisaidia
pia kuimarisha ulinzi wa eneo hilo.
Kwa kuwa vijana hao walikaa
nje ya nyumba kwa muda mrefu hadi usiku wa manane, eneo hilo liliendelea
kuwa na shughuli na watu, jambo lililofanya iwe vigumu kwa wezi kuvamia
nyumba hiyo bila kuonekana au kugundulika.
Kwa njia hiyo, vijana
hao wakajikuta wakifanya kazi kama walinzi wa nyumba hiyo bila kujua,
huku wao wakifurahia huduma ya intaneti bure.
Mkakati huo
ulimsaidia mwenye nyumba kupata ulinzi wa ziada wakati akiendelea na
mpango wa kuajiri mlinzi rasmi.Tangu aanze kutumia mbinu hiyo, nyumba
yake haijawahi kukumbwa na tukio la wizi.
Hatua hiyo imeonyesha
namna ubunifu na matumizi ya teknolojia yanavyoweza kutumika kutatua
changamoto za usalama, huku huduma iliyoonekana kuwa ya kawaida ya Wi-Fi
bure ikigeuka kuwa sehemu ya mkakati wa kulinda nyumba.
0 Comments