ACHOMA MOTO JENGO LA MAHAKAMA YA MWANZO-MOSHI

 Mtu mmoja anayedaiwa kuwa na tatizo la ugonjwa wa akili amechoma moto kwa jengo la zamani la Mahakama ya Mwanzo Moshi, mkoani Kilimanjaro, na kusababisha vyumba vinane (8), nyaraka za Mahakama pamoja na sehemu ya jengo la Ustawi wa Jamii kuteketea kwa moto.

Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Kilimanjaro, Jeremia Mkomangi, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema askari wa zimamoto walifika katika eneo la tukio na kufanikiwa kuuzima moto huo.

Kwa mujibu wa Mkomangi, moto huo ulisababisha kuungua kwa ofisi moja ya jengo hilo pamoja na chumba kilichokuwa kikihifadhi nyaraka za mahakama, na kusababisha nyaraka zilizokuwamo kuteketea.

Amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa moto huo ulisababishwa kwa makusudi, huku mtu mmoja anayesadikiwa kuwa na changamoto za afya ya akili akihusishwa na tukio hilo.

“Vyumba vinane vya Mahakama ya Mwanzo pamoja na nyaraka zake zote na jengo la Ustawi wa Jamii Moshi vimeungua. Chanzo cha moto huo ni kuchomwa kwa makusudi na mtu anayesadikiwa kuwa na tatizo la akili,” amesema Mkomangi.

Post a Comment

0 Comments