Mwanafunzi wa
kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Rudewa, Athuman Salum (16),
amefariki dunia baada ya kushambuliwa na mamba akiwa katika shughuli za
uvuvi kwenye Mto Wami uliopo wilayani Kilosa.
Tukio hilo
limetokea katika eneo la Kijiji cha Rudewa Batini na kuacha huzuni kubwa
kwa familia, wanafunzi pamoja na wakazi wa kijiji hicho.
Mwenyekiti
wa Kijiji cha Rudewa Batini, Masoud Msabaha, amesema kijana huyo
alikuwa ameenda kuvua samaki mtoni kabla ya kushambuliwa ghafla na
mnyama huyo hatari.
Alieleza kuwa wananchi waliinua juhudi za
kumtafuta marehemu mara baada ya tukio kutokea, lakini sehemu pekee
iliyopatikana ni kichwa chake, ambacho tayari kimezikwa kwa taratibu za
mazishi.
Baada ya tukio hilo, Kamati ya Usalama ya Wilaya ya
Kilosa ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya, Shaka Hamdu Shaka, ilitembelea eneo
la tukio na kuagiza kuwekwa kwa alama za tahadhari kuonyesha hatari ya
uwepo wa mamba katika Mto huo.
Mkuu huyo wa wilaya amewataka
wananchi kuwa waangalifu wanapotumia au kuvuka mto huo, akieleza kuwa
taarifa zilizopo zinaonyesha eneo hilo lina idadi kubwa ya mamba.
0 Comments