Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam Ndg Abdul R. Mhinte leo Januari 30,2026 ameongoza kikao cha tathimini ya utendaji kazi katika taasisi za umma Mkoani humo ambacho kimefanyika katika Ukumbi wa Iddy Nyundo na kuhudhuriwa na Sekretarieti ya Mkoa, Watendaji wakuu wa taasisi za umma pamoja na Wakurugenzi wa Halmashauri zote tano za Mkoa.
Akifungua kikao hicho Ndg Mhinte ametoa shukrani kwa taasisi za umma kwa kushiriki kikamilifu kipindi cha uchaguzi mkuu 2025 ambapo amesema tumemaliza shughuli za uchaguzi kilichobaki sasa kuchapa kazi kwa bidii ili kuwaletea wananchi maendeleo.
Aidha Katibu Tawala wa Mkoa alianza na kuongoza kujadili masuala ya kimaendeleo katika Mkoa hususani namna bora ya kuratibu mazingira rafiki ya wafanyabiashata eneo la Karikoo, Bodaboda na Machinga ambapo baada ya mjadala yakapatikana na maazimio ambayo yatakwenda kuweka mazingira bora ya ufanyaji biashara kwa makundi yote katika eneo la Karikoo.
Vilevile kupitia kikao hicho taasisi mbalimbali ziliwasilisha taarifa za utendaji kazi kwa kipindi cha robo mwaka, taasisi hizo ni kama Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, TRA, Hospitali ya Amana, DAWASA, TANESCO, TARURA,NEMC,TANROAD, Bonde la mto wami, LATRA, TAZAMA, UDART, MSD, Hospitali ya Rufaa Temeke, Hospitali ya Rufaa Mwananyamala, Bandari, TBS, Shirika la Masoko Kariakoo, Wakala wa Vipimo na NSSSF
Sanjari na hilo Katibu Tawala wa Mkoa ametoa wito kwa taasisi za umma ndani ya Mkoa kujenga utamaduni wa kuwa na mawasiliano wakati wote zinapotekeleza majukumu yake hususani utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo pia kuhakikisha miradi yote inayotekelezwa katika maeneo yao inajulikana vizuri kwa wananchi ni wakati muafaka wa kuhakisha taarifa za utekelezaji wa miradi zinawafikia wananchi kwa wakati.





0 Comments