WANAOCHOCHEA TAHARUKI WANAUME 'KUPOTEZWA NYETI' WAONYWA VIKALI

 Kufuatia taarifa zinazozunguka mitandaoni kuhusu wanaume Tunduma kudaiwa kupotezewa nyeti zao kwa imani za kishirikina, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Jabiri Makame, ametoa onyo kali kwa yeyote anayesambaza uvumi huo na kwamba atakayekiuka amri hiyo atachukuliwa hatua.

Makame ametoa onyo hilo wakati akizungumza na wananchi katika eneo la Kilimanjaro, Halmashauri ya Mji wa Tunduma, akisisitiza kwamba imani za kishirikina zinachangia kuibuka kwa matukio yanayoweza kusababisha kusimama kwa shughuli za kiuchumi na maendeleo.

Amebainisha kuwa asilimia kubwa ya walioarifu kupotezewa nyeti zao walikaguliwa na kupatikana wazima, hivyo kuendeleza taarifa hizo ni kuchochea taharuki na kusimamisha maendeleo.

Aidha, amewataka wananchi wa Tunduma kuacha kueneza imani za kishirikina na badala yake wajikite katika kazi na shughuli za maendeleo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Augustino Senga, amesema tayari watu 26 wako mikononi mwa polisi kutokana na matukio ya uchochezi.

Baadhi ya wananchi, akiwemo Rehema Ngonya, wamedai kwamba matumizi ya dawa za kuongeza nguvu za kiume, ikiwemo “Vumbi la Congo”, ni moja ya sababu zinazoathiri maumbile yao, huku vijana wengi wakitumia dawa hizo bila uangalifu. Ziara ya Mkuu wa Mkoa ililenga pia kutoa taarifa ya hali ya usalama kuelekea Sikukuu ya Pasaka.


 

Post a Comment

0 Comments