Ushirikiano
baina ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Walipakodi umetajwa
kuwezesha Mamlaka hiyo kuandika historia mpya kwa kukusanya kiasi cha
shilingi trilioni 9.31 kwa kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha
2025/26 sawa na ufanisi wa asilimia 106.4 ya lengo la kukusanya shilingi
trilioni 8.75.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamishna
Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda April 1, 2026 imeeleza kuwa kwa mwezi
Machi pekee TRA imekusanya shilingi trilioni 3.58 sawa na ufanisi wa
asilimia 107.6 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 3.32.
Taarifa
hiyo imeeleza kuwa makusanyo hayo ya kipindi cha robo ya tatu ya mwaka
wa fedha 2025/26, ni sawa na ukuaji wa asilimia 23.6 ikilinganishwa na
kiasi cha shilingi trilioni 7.53 kilichokusanywa katika kipindi kama
hicho mwaka wa fedha 2024/25.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo Ufanisi
wa makusanyo kwa mwezi Machi unapelekea TRA kuweza kuandika rekodi mpya
za kipekee katika ukusanyaji wa mapato nchini Wastani wa Makusanyo kwa
mwezi katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26 umefikia shilingi
trilioni 3.10 ambacho ni kiasi cha juu kabisa ukilinganisha na wastani
wa shilingi trilioni 2.51 kwa kipindi kama hicho mwaka 2024/25.
TRA
imeweza kurekodi Ukuaji chanya wa asilimia 23.6 katika kipindi cha
Januari -Machi 2026, na imeweza kulifikia na kuvuka lengo la makusanyo
kwa miezi 21 mfululizo kuanzia mwezi Julai 2024, mafanikio ambayo
Mamlaka haijawahi yafikia toka ianzishwe hali ambayo imechagizwa na
makusanyo ambayo yamechangiwa na ukaribu uliopo baina ya Mamlaka hiyo na
Walipakodi.
Imeeleza kuwa Makusanyo yaliyokusanywa kwenye robo
ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2025/26 ni sawa na ukuaji wa asilimia 114.1
ukilinganisha na kiasi cha shilingi trilioni 4.35 kilichokusanywa katika
kipindi kama hicho wakati Serikali ya Awamu ya Sita ilipoingia
madarakani, mwaka 2020/21.
Ushirikiano baina ya TRA na
walipakodi umeiwezesha katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026,
kusajili walipakodi waруа 900,755 ambao ni ufanisi wa asilimia 131.36 wa
kusajili walipakodi wapya 685,706 kufikia tarehe 31 Machi, 2026.
0 Comments