Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, ameshuhudia Utiaji Saini wa Mkataba wa uendelezaji wa leseni za utafiti wa madini ya Kinywe (Graphite) kati ya Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na Kampuni ya Planet One Natural Resources Holdings PTE LTD ya Singapore.
Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Kiruswa amesema mkataba huo ni hatua muhimu itakayochochea maendeleo endelevu katika eneo la Mirerani, Wilaya ya Simanjiro na Mkoa wa Manyara kwa ujumla.
Amesisitiza kuwa utekelezaji wa mradi huo unapaswa kuwanufaisha wananchi wa eneo husika kwa kuwapa kipaumbele katika ajira pamoja na kushirikishwa kikamilifu katika shughuli za kiuchumi zinazotokana na mradi huo.
“Ni muhimu kuhakikisha wafanyakazi wanatoka Mirerani na maeneo ya jirani, lakini pia kampuni zinunue bidhaa na huduma kutoka Simanjiro ili kuongeza mzunguko wa fedha kwa wananchi,” amesema Dkt. Kiruswa.
Aidha, amesema madini ya Kinywe ni madini mkakati yenye mahitaji makubwa duniani, hususan katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, hivyo kutoa fursa adhimu kwa Tanzania kiuchumi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Dkt. Venance Mwasse, amesema shirika hilo linaendelea kuvutia uwekezaji mkubwa katika sekta ya madini, huku akibainisha kuwa huu ni mkataba wa tatu kusainiwa ndani ya mwaka huu.
“Hii inaonesha wazi kuwa Tanzania imeendelea kuwa kivutio cha uwekezaji katika sekta ya madini. Mradi huu utazalisha ajira nyingi, hususan kwa wananchi wa Mirerani,” amesema Dkt. Mwasse.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO, Balozi Simon Sirro, amesema uwekezaji huo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha uchumi wa wananchi kupitia rasilimali za madini.
Amewataka wananchi wa Simanjiro kushirikiana na wawekezaji pamoja na kuzingatia uadilifu, hasa kwa wale watakaopata fursa za ajira katika mradi huo.






0 Comments