MGORE ASAKWA NA JESHI LA POLISI KWA MAUAJI YA MUMEWE MKOANI MWANZA

 Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linamsaka mwanamke mmoja aliyetambuliwa kwa jina moja la Mgore anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 25 na mkazi wa Ibanda, Kata ya Kirumba Wilaya ya Ilemela kwa tuhuma za mauaji ya mume wake aitwaye Amosi Faustine Paulo, miaka 31, dereva wa pikipiki na mkazi wa Ibanda aliyeuawa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali kichwani upande wa kisogoni.

 

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi leo Juni 27, 2025 tukio hilo limetokea Juni 25,2025 majira ya saa 4.30 usiku huko katika hospitali ya Mkoa wa Mwanza, Sekou-Toure muda mchache wakati Amosi Faustine Paulo alipofikishwa kwa ajili ya kupatiwa matibabu ili kuokoa maisha yake baada ya kujeruhiwa na kitu chenye ncha kali na mke wake wakiwa chumbani kwenye nyumba ya Joseph Bukoma Misungwi iliyopo eneo la Ibanda, Wilaya ya Ilemela walipokuwa wamepanga.

Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi sambamba na kumsaka mtuhumiwa aliyetoroka baada ya kutenda tukio hilo ili aweze kuchukuliwa hatua za kisheria. Mwili wa marehemu umefanyiwa uchunguzi wa kitaalamu na kukabidhiwa ndugu kwa taratibu za mazishi.

Aidha, chanzo cha tukio hilo ni wivu wa kimapenzi kwani inadaiwa mwanamke huyo alikuwa akimtuhumu mume wake kuwa na mahusiano ya kimapenzi na wanawake wengine.

Post a Comment

0 Comments